Usikose Hizi Hapa

RAIS MAGUFULI AREJEA JIJINI DAR ES SALAAM

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli tarehe 15 Oktoba, 2017 amerejea Jijini Dar es Salaam akitokea Zanzibar ambako jana alikuwa mgeni rasmi katika sherehe za kilele cha mbio za Mwenge wa Uhuru, kumbukumbu ya Hayati Baba wa Taifa Mwl. Julius Kambarage Nyerere na wiki ya vijana zilizofanyika katika uwanja wa Amaan Mjini Magharibi.
Katika uwanja wa ndege wa kimataifa wa Abeid Amani Karume, Mhe. Rais Magufuli ameagwa na viongozi wa Mkoa wa Mjini Magharibi wakiongozwa na Mkuu wa Mkoa huo Bw. Ayoub Mohamed Mahmoud.

Kabla ya kuondoka Ikulu Zanzibar Mhe. Rais Magufuli amekula chakula cha mchana na wakimbiza Mwenge wa Uhuru mwaka huu walioongozwa na Amour Hamad Amour na kuwahakikishia kuwa Serikali itafanyia kazi taarifa ya Mwenge waliyoiwasilisha kwake katika sherehe za jana.

“Mlipokuwa mkikimbiza Mwenge wa Uhuru nilikuwa nafuatilia miradi mliyokuwa mnatembeleana maelekezo mliyokuwa mkitoa, sehemu zote mlizobaini kuwepo kwa dosari ninawahakikishia kuwa tutazifuatilia na kuchukua hatua” amesema Mhe. Rais Magufuli.

Mhe. Rais Magufuli amesema anatambua uzalendo waliouonesha wakati wote wa kukimbiza Mwenge wa Uhuru na amewasihi kuendeleza maadili na uzalendo huo kwa manufaa ya taifa.

Kwa upande wao wakimbiza Mwenge hao wamemshukuru Mhe. Rais Magufuli kwa heshima kubwa na upendo aliyowaonesha, kwa kupokea taarifa yao na kuahidi kuifanyia kazi na pia kuwaalika kula nao chakula cha mchana kwa kuwa hii imekuwa ni historia ya kipekee kwa wakimbiza Mwenge wa Uhuru hapa nchini.

Gerson Msigwa
Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, IKULU
Zanzibar
15 Oktoba, 2017

No comments