Usikose Hizi Hapa

MATUKIO YA KIHALIFU YAMEPUNGUA MWAKA HUU - DCI ROBERT BOAZ

Jeshi la Polisi limesema matukio ya kihalifu kwa mwaka huu,yamepungua kutoka 68,204 yaliyoripotiwa mwaka 2016 hadi kufikia matukio 61,774 kwa mwaka 2017 huku likisema hali ya usalama imezidi kuimarika.

Kauli hiyo imetolewa na Mkurugenzi wa makosa ya jinai -DCI, Robert Boaz alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari juu ya muenendo wa hali ya Usalama wa nchi hususani kuelekea mwishoni mwa mwaka.

Akizungumzia tukio la kupotea kwa mwandishi wa Gazeti la Mwananchi,Azory Gwanda,Boaz amesema wanachukua kila hatua, na kuwaomba wananchi wawe na subira wakati jeshi linaendelea kuchukua taratibu zinazotakiwa.

Pia amesema uchunguzi wa kushambuliwa mbunge wa Singida Mashariki Tundu Lissu na kesi za tuhuma za uchochezi zinazomkabili Mjumbe wa kamati kuu ya Chadema,Edward Lowassa bado unaendelea.

Kwa upande wa  makosa ya usalama  barabarani  DCI- Boaz 
amesema yamepungua  kutokana na  matukio  yaliyoripotiwa  ni  9,550  katika kipindi cha januari mpaka novemba  mwaka 2016 ikilinganishwa na na matukio 5,537 yaliyoripotiwa katika kipindi  kama hicho mwaka 2017 ambapo kuna upungufu wa  matukio 4,013 sawa na asilimia 42.


 Ajali hizo  zilisababisha  vifo vya watu  3,108 na majeruhi 8,898 kwa mwaka  2016 wakati mwaka huu 2017  vifo vya watu ni  2,491 na majeruhi 5,696

Hata hivyo ameongeza kuwa pamoja na uhalifu kupungua mwaka huu,bado kuna changamoto za makosa  dhidi ya binadamu ambayo  yanajumuisha ubakaji,kulawiti, wizi wa watoto  mauaji ,kunajisi pamoja na kusafirisha  binadamu ambapo makosa hayo ya jinai yameongezeka  kutoka   11,513 mwaka 2016 hadi kufikia 11,620 mwaka huu 2017 ambayo ni ongezeko la makosa 107  sawa  na asilimia  0.9.


No comments