Usikose Hizi Hapa

Joshua Nassari Apeleka vielelezo vingine Takukuru

Mbunge wa Arumeru Mashariki, Joshua Nassari amewasilisha vielelezo vingine katika Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) ili kuthibitisha tuhuma za rushwa dhidi ya viongozi wa Serikali wanaodaiwa kuwanunua madiwani wa Chadema waliohamia CCM.
Nassari aliwasili katika ofisi hizo jana saa 7:57 mchana na kutoka saa 11:33 jioni.

Wakati Nassari akiendelea na mahojiano hayo, maofisa wa Takukuru waliwafukuza waandishi wa habari waliokuwa katika eneo hilo wakisubiri kufanya mahojiano na mbunge huyo.

Hata alipotoka alikuwa amesindikizwa na maofisa hao waliokuwa wakiwazuia waandishi ambao waliamua kumsubiri nje ya lango la ofisi hizo wasifanye mahojiano.

Mmoja wa maofisa hao alimsindikiza mbunge huyo hadi alipohakikisha ameingia ndani ya gari na kuondoka eneo hilo.

Nassari aliwataka waandishi wamfuate katika eneo jingine kwa ajili ya mahojiano.

Akieleza sababu za mahojiano yake kuchukua muda mrefu, Nassari alisema hilo limesababishwa na wingi na uzito wa vielelezo alivyokuwa navyo.

“Nimewasilisha vielelezo na nimefungua jalada, nikatoa maelezo yangu mengine nimewaachia wao waendelee na uchunguzi.

“Ushahidi nilionao ni mkubwa mno umehusisha viongozi wengi, nami nimetoa kila nilichonacho na kuna nyaraka nyingine zipo Arusha zikifika kwa wakati muafaka nitaziwasilisha,” alisema.

No comments