Usikose Hizi Hapa

WATAKWIMU NCHINI KUTUMIA TEKNOLOJIA YA KISASA KATIKA UKUSANYAJI WA TAKWIMU BORA

Watakwimu nchini wametakiwa kuimarisha mbinu za uzalishaji wa takwimu kwa kutumia teknolojia za kisasa ili kusaidia katika ukusanyaji na upatikanaji wa takwimu bora zitakazosaidia kupanga mipango ya maendeleo.


Hayo yamesemwa leo Jijini Dar es Salaam na Mkurugenzi wa Uchumi kutoka Benki Kuu ya Tanzania, Johnson Nyala wakati wa maadhimisho ya Siku ya Takwimu Afrika na kuwataka wadau waliopo kwenye mfumo wa utoaji na utumiaji wa takwimu kushirikiana ili kupunguza kukosekana kwa ulinganifu wa takwimu.

“Matumizi ya teknolojia yataipunguzia Serikali gharama za uzalishaji wa takwimu na kuongeza ubora kutokana na mahitaji makubwa ya takwimu kwa matumizi mbalimbali,” alisema Bw. Nyala.

Nyila aliongeza kuwa takwimu bora za uchumi ni muhimu katika kupanga mipango ya maendeleo na utungaji wa sera kwa ajili ya kuboresha maisha ya wananchi.

“Wakati nchi mbali mbali duniani ikiwemo Tanzania zimeanza kutekeleza agenda ya maendeleo endelevu ya mwaka 2030, mahitaji ya takwimu bora za uchumi yanahitajika sana,” alisema Bw. Nyila.

Kwa upande wake Mkurugezni Mkuu wa Ofisi ya Taifa ya Takwimu, Dkt. Albina Chuwa amesema kuwa madhumuni makubwa ya kuadhimisha siku hii ni kuongeza uelewa wa umma juu ya umuhimu wa takwimu katika nyanja zote za kimaisha ya kijamii na kiuchumi. 

Ameongeza kuwa nchi mbalimbali za Afrika zilikubaliana kuadhimisha maadhimisho hayo kutokana na uhitaji mkubwa wa ukusanyaji, uchambuzi na usambazaji wa takwimu za uchumi katika kuelekea utekelezaji wa Agenda ya Afrika ya mwaka 2063 na malengo ya maendeleo endelevu ya mwaka 2030. 

Siku ya Takwimu Duniani huadhimishwa tarehe 20 Oktoba katika kipindi cha kila miaka mitano ambapo kwa mwaka huu maadhimisho haya yameongozwa na Kauli mbiu isemayo “Takwimu Bora za Uchumi kwa  Maisha Bora”.

No comments