Usikose Hizi Hapa

UHAMIAJI WAPEWA SIKU TATU KUHAMA MJINI

Idara ya Uhamiaji katika Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi imetoa siku tatu kwa watumishi wake walioripoti Dodoma kuhamia katika nyumba zake zilizopo eneo la Iyumbu, nje kidogo ya Manispaa ya Dodoma, badala ya kung’ang’ania kuishi katikati ya mji.

Nyumba hizo 63 zenye thamani ya Sh. bilioni 3.8 zimekabidhiwa jana kwa Idara hiyo na Shirika la Nyumba (NHC).

Akizungumza katika makabidhiano hayo, Kamishna wa Fedha wa Idara hiyo, Peter Chogero, kwa niaba ya Kamshina Mkuu alisema serikali imeshanunua nyumba kwa ajili ya watumishi hao hivyo hakuna sababu ya wao kuendelea kuishi katikati ya mji wa Dodoma.

“Uhamiaji imenunua nyumba 63 eneo la Iyumbu ambazo zimejengwa na NHC, tutashangaa kuona watumishi wengine waendelee kuishi mjini wakati nyumba zao zipo hapa Iyumbu,” alisema.

Alitoa siku tatu kuanzia jana kila mtumishi aliyepangwa kuhamia kwenye nyumba hizo awe ameingia kwa kuwa hakuna sababu ya kung’ang’ania kuishi nje ya nyumba hizo wakati zimelipiwa na serikali.

Chongero alisema kabla ya manunuzi ya nyumba hizo, Idara hiyo ilikuwa na nyumba 10 mjini Dodoma ambazo hazikuweza kutosheleza watumishi wote, ikiwamo waliohamia kutoka Makao Makuu Dar es Salaam.

Alibainisha waliamua kuongeza idadi ya nyumba ili kila mtumishi wa Uhamiaji aishi kwenye nyumba ya serikali na kwamba wanatarajia kuongeza nyingine 40.

Naye, Meneja Masoko wa NHC, Itandula Gambalagi alisema ujenzi wa nyumba za Uhamiaji ulianza Desemba, 2016 katika eneo lenye ukubwa wa ekari 234 na ni moja ya sehemu ya mji uliopangiliwa kitaalamu kwa kuzingatia sheria na kanuni za mipango miji.

Alisema nyumba zilizokabidhiwa Uhamiaji ni sehemu ya nyumba 150 zilizojengwa katika mradi wa Iyumbu na tayari nyumba zilizobaki zote zimepata wanunuzi.

Gambalagi alisema nyumba hizo zina miundombinu yote inayotakiwa.

Kwa upande wake, mthamini wa mali za serikali, Joseph Maliti aliagiza Uhamiaji kuingiza nyumba hizo katika daftari la mali za serikali mara moja, ikiwa ni pamoja na thamani kwa kila nyumba.

No comments